Staa wa Bongo Movie, Komediani kipenzi cha wengi Bongo, Majuto
Athuman ‘Mzee Majuto’, anadaiwa kuzama kwa mara nyingine kwenye penzi la
msichana mbichi anayekadiriwa kuwa na umri sawa na mjuu wake.
Akizungumza na gazeti la Ijumaa Wikienda, wikiendi iliyopita, mke wa
Mzee Majuto aitwaye Aisha Yusuf alikiri kuwa mumewe amenasa kwa
‘kibinti’ chenye umri wa miaka 18.
Aisha alidai kwamba, Mzee Majuto anaishi na binti huyo kama mke na mume,
jambo ambalo watu wamekuwa wakimshangaa na kuhoji kwa nini anatoka na
mtoto mdogo kiasi hicho wakati ana watoto wakubwa wenye uwezo wa kuzaa
msichana kama huyo na akawa mjukuu wake.
“Kinachonichosha mimi kwa nini anafanya hivyo wakati yeye ni kioo cha jamii?
“Watu wengi wanatakiwa kujifunza mengi kupitia kwake, maana tangu aoe
hata sisi hatujafurahishwa na jambo hilo ingawa kweli ni uamuzi wake.
“Kingine amekuwa hakai tena hapa nyumbani (Tanga) na kuna kipindi
unapita hata mwezi tunawasilia kwenye simu tu labda mtoto aumwe ndiyo
atapita tu na siyo kukaa.
“Sijui mzee wangu anafanya hivyo kwa nini maana sasa ana zaidi ya
miaka 60 na kama mtoto mimi sasa hivi nina umri wa miaka 35 kwake bado
mimi mdogo sana na nina umri wa watoto wake wa kuzaa sasa huyo aliyemuoa
si ni mjukuu wake kabisa?
“Mimi naona aibu tu kama familia ingawa dini kweli inaruhusu lakini si kwa mtoto kama yule,” alisema Aisha kwa uchungu.
Baada ya kumsikia mkewe, gazeti hilo lilimtafuta Mzee Majuto ili
azungumzie ishu hiyo ambapo simu yake ilipokelewa na msichana mwenye
sauti nyororo huku akidai kwamba mzee Majuto amelala apigiwe baadaye.
“Mimi ni mke wake mdogo, Mzee Majuto amelala, nafikiri jaribu kupiga
baadaye anaweza kuwa ameamka na utaweza kuzungumza naye vizuri,”
alisema.
Mzee Majuto alipotafutwa baadaye, simu yake iliita bila kupokelewa.
Baadhi ya wasanii waliozungumza na gazeti hili kwa sharti la
kutotajwa majina yao walilaani kitendo cha Mzee Majuto kuwa na binti
huyo kwani umri wake umeenda.