MSANII wa filamu za Kibongo, Doreen Reguna ‘Queen Magali’ amefunguka
kuwa kifo cha staa wa Bongo Fleva, Moses Mshagama ‘Mez B’ ni pigo kubwa
sana kwake kwani marehemu alikuwa ni mpenzi wake na alikuwa na mimba
yake.
Akizungumza na gazeti hili huku akionesha sura ya masikitiko, Queen
Magali alisema kinachomuuma zaidi ni kwamba, ujauzito wa marehemu
aliokuwa nao, ulichoropoka saa chache baada ya kupokea taarifa za msiba
huo.
“Nilipopigiwa simu kwa mara ya kwanza, sikuamini, hata ndugu zake
marehemu walinipigia simu, sikuamini hadi nilipompigia shangazi yake
ambaye alinithibitishia msiba huo, hapohapo nikapata mshutuko, hali
yangu ikawa mbaya hadi nikalazwa.
“Nashukuru Mungu kwa sasa naendelea vizuri.
“Kiukweli msiba huu kwangu umekuwa ni pigo kubwa, tulikuwa na mipango
mingi na marehemu katika maisha yetu, alishanitambulisha kwa ndugu na
jamaa zake wote wa karibu lakini nasikitika zaidi kwa kuwa nimechelewa
kuhudhuria mazishi ya mpenzi wangu kutokana na kuzidiwa ghafla lakini
nitafanya kila liwezekanalo ili nikaweke japo mchanga kwenye kaburi la
mtu niliyempenda katika maisha yangu,” alisema Queen Magali.
Baadhi ya wapenda ‘ubuyu’ waliokuwa wakisikiliza mahojiano ya Queen
Magali na mwanahabari wetu, walisikika wakihoji kwa nini mrembo huyo
asianike uhusiano wake na Mez B kabla hajafariki lakini mwenyewe alidai
walikubaliana uchumba wao uwe wa siri.
Mez B alifariki dunia nyumbani kwao Dodoma Ijumaa iliyopita ambapo alizikwa katika makaburi ya Wahanga wa Reli, Dodoma.