Septemba 30, 2015 Jijini Mbeya: Kampuni
ya Tigo Tanzania kwa kushirikiana na shirika lisilokuwa la kiserikali
linalotoa misaada katika jamii lijulikanalo kama Hassan Maajar Trust
(HMT) wametoa mchango wa madawati 700 yenye thamani ya shilingi za
kitanzania milioni 49 kwenye shule za msingi 32 katika wilaya ya
Rungwe, Mbozi na wilaya ya Mbeya Mjini.
Akizungumza
katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika katika moja ya shule jijini
Mbeya, Meneja Mkuu wa Tigo, Diego Gutierrez alisema: “ mchango huu ni
sambamba na dhamira ya kampuni ya kuunga mkono mipango ya kijamii
kupitia wigo wake wa kushirikisha jamii”.
“Kupitia
mchango huu, kampuni ya Tigo inawajibika katika kutengeneza viongozi wa
baadaye wakiwamo madaktari, wahandisi na wataalamu wengine wa nchi hii,
"alisema Gutierrez.
Alisema,
katika miezi ya hivi karibuni kampuni ilitoa mchango kama huo wa
madawati katika mikoa ya Iringa na Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya ahadi
ya dola za Marekani 50,000 kwa serikali, ahadi ambayo kampuni ya Tigo
ilitoa mwaka jana ili kusaidia kukabiliana na uhaba wa madawati katika
shule za umma nchini.
Makabidhiano
yalishuhudiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro ambaye alisema
madawati hayo700 yataboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto katika
wilaya hizo tatu, akitoa wito kwa wadau wengine wenye mapenzi mema
kujitolea na kujiunga kwenye jitihada za kukabiliana na sehemu iliyobaki
ya uhaba wa madawati mkoani humo.
Picha na habari kwa hisani ya http://bongodailyupdates.blogspot.com/