Richard Bukos na Makongoro Oging’/Uwazi
Habari
zilizolitikisa Jiji la Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita ni
pamoja na ile ya mkazi wa Chamazi, Hussein Mfaume, kumchoma visu hawara
yake, Ester Thomas Ungele (30), naye kujichoma mpaka kujitoa utumbo,
Uwazi limeichimba kwa kina.
Habari zilidai kuwa, kisa hasa cha mwanaume huyo kujichukulia uamuzi
huo wa kikatili ni madai ya mwanamke huyo kuwa na uhusiano wa
kimapenzi na mwanaume mwingine anayedaiwa kuwa ni dereva wa teksi.
MANENO YA SHUHUDA MKUU
Kwa mujibu wa shuhuda wa tukio hilo
ambaye ni mtoto wa Ester, Sarah siku hiyo, yeye na mama yake walikuwa
kwenye eneo lao la biashara ya Mama Lishe, nje ya Ukumbi wa Vijana,
Amana uliopo Ilala, Dar.
“Ghafla nilimwona Hussein akija huku usoni akionekana mtu mwenye
hasira. Alimfuata mama alipokuwa na kumuuliza ni kwa nini anamfanyia
dharau?”
MALUMBANO YAANZA, WAKIMBIZANA
Sarah anaendelea: “Niliona kama
malumbano ya kawaida nikawa nawaangalia lakini nikashangaa kumuona
Hussein akimsogelea mama na kutoa kisu.“Mama alianza kukimbia naye
Hussein akamkimbiza huku bado ameshika kisu mkononi. Niliogopa sana,
nikatetemeka. Nilipiga mayowe kumuombea msaada mama.
“Mama alikimbia uelekeo wa kuingia kwenye Ukumbi wa Vijana lakini
kabla hajafika, Hussein alimchota mtama mama akaanguka. Ndipo Hussein
alipoanza kumchoma visu mama sehemu mbalimbali za mwili na kisha kumkita
nacho kichwani.”
KISU MWILINI MWAKE
Sarah tena: “Baada ya kumchoma mama visu
hivyo, nilishangaa kumuona Hussein na yeye akijichoma visu sehemu
mbalimbali za mwili wake lakini mwisho alijikita nacho tumboni na kuanza
kukitikisa kama vile alikuwa anauchanachana utumbo wake, akaishiwa
nguvu na kuanguka. Ndipo wasamaria wema wakaanza kuwasogelea.”
Sarah alisema hata yeye alisogea eneo hilo na kuwakuta wote
wamepoteza fahamu huku utumbo wa mwanume ukiwa nje na damu chapachapa
ikiwa imetapakaa mwilini. Wakachukuliwa na kukimbizwa Hospitali ya Mkoa
wa Ilala, Amana, Dar ambapo ni mita chache tu kutoka eneo la tukio.
MKE WA HUSSEIN SASA
Naye mke wa mtuhumiwa huyo aliyejitambulisha
kwa jina la Zubeda Abeid alipopata nafasi ya kuzungumza na Uwazi alikuwa
na ya kusema:“Ukweli taarifa hizi nimezipata kwa mshtuko mkubwa sana
hali iliyonifanya nipoteze fahamu. Hussein ni mume wangu wa ndoa,
alinioa mwaka 1997 kijijini kwetu, Likombora mkoani Lindi. Tuna watoto
wanne.
”Mwaka 2003 tulihamia hapa Dar kutafuta maisha zaidi ya Lindi,
mwenzangu kazi yake ikiwa ni kuuza kahawa pale karibu na huyo hawara
yake aliyemchoma visu. Mimi ni mama wa nyumbani tu.
“Sijui
walihitilafiana kitu gani na huyo hawara yake maana leo ndiyo nimejua
kumbe mume wangu alikuwa na hawara. Lakini hebu soma meseji hii kwenye
simu yangu, alinitumia mume wangu mwanzoni mwa mwezi huu (Februari) bila
kuhofia kuwa mimi ni mke wake.”
ILIVYOSOMEKA MESEJI
“MAMA NEEMA NAKUOMBA MESEJI HIYO ISOME PEKE
YAKO NA USIMWAMBIE MTU YEYOTE. MIMI NAJIUA KWA SABABU ESTER HANITAKI.
WEWE BAKI NA WATOTO, NIMEVUMILIA KUKUFICHA NIMESHINDWA. KWA HIYO MIMI
NAJINYONGA, WEWE BAKI NA WATOTO.”
Baada ya Uwazi kuzungumza na mwanamke huyo, lilibahatika kuzungumza
na dalali mmoja wa magari anayefanyia shughuli zake eneo hilo lakini
aliomba jina lake lisiandikwe gazetini.
“Hussein alikuwa akimtuhumu
dereva taksi mmoja kwamba anaingilia penzi lake na mwanamke huyo
aliyemjeruhi na amekuwa akiahidi kulipa kisasi.
“Yaani leo kama jamaa angekuwepo hapa basi ndiye angekuwa wa kwanza
kuchomwa visu, pengine huyu mwanamke angefuatia,” alisema dalali huyo
aliyeshuhudia tukio hilo.
MGANGA MKUU
Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Mganga Mkuu wa
Hospitali ya Amana, Dk. Shaany Mwaruka alikiri kuwapokea majeruhi hao na
kusema: “Kwa sasa hali za majeruhi zinaendelea vizuri ingawa awali hali
ilikuwa mbaya na kusababisha wakimbizwe chumba cha upasuaji kutokana na
kisu kilichotumika kuingia sana ndani ya miili.”