BONGOCLAN Tanzania

Website yetu ipo katikamatengenezo

Copyright © BongoClan Tanzania™ | Published By Gooyaabi Templates | Powered By Blogger
Design by WebSuccessAgency | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com

HABARI ZILIZOSOMWA SANA WIKI HII

Wema ni kweli anavuta Bangi???

SIKU chache baada ya picha za mtoto mchanga kusambazwa katika mitandao ya kijamii na kudai kuwa ni za mtoto wa mwimbaji wa nyimbo za Injili nchini, Flora Mbasha kuwa amezaa na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima hatimaye wawili hao wamefunguka.

Hatua hiyo imekuja miezi saba tangu wawili hao walipoingia katika mgogoro wa ndoa yao hali iliyosababisha mume wa Flora, Emmanuel Mbasha kufikishwa mahakamani kwa kosa la ubakaji.
Akizungumza na MTANZANIA jijini Dar es Salaam jana ili kupata ukweli kuhusu taarifa za picha za mtoto huyo ambaye anadaiwa kuwa amezaa na Flora, Mchungaji Gwajima, alisema taarifa hizo ni za uzushi na huenda zinasambazwa na mume wa Flora.

Mchungaji Gwajima alikwenda mbali na kusema pamoja na uzushi huo unaosambazwa dhidi yake kwa kuhusishwa katika uhusiano na Flora anamwachia Mungu kila kitu.

“Hahaha… si unajua hiyo issue (suala, jambo) ya Mbasha ni ya muda mrefu tu… wakati mwingine mimi huwa sijibu ujinga,” alisema Gwajima huku akicheka.
“Awali niliwaza kuwashitaki (alipoanza kuhusishwa kwamba ana uhusiano na Flora) wanaoeneza uzushi huo lakini nikaona ‘It doesn’t hold water’ (haina mashiko), najua shutuma hizo zinatoka wapi,” alisema Mchungaji Gwajima.

Alipoulizwa kuhusu mtu anayemshuku kueneza uvumi huo alisema: “Probably’ (nadhani) atakuwa Emmanuel Mbasha mwenyewe. Tangu mwanzo alipotuhumiwa kumbaka shemeji yake na kutoroka kwake akihofia kukamatwa na polisi, mkewe alikuja kanisani kwetu na mimi nilimwagiza mwenyekiti wa kusaidia jamii amsaidie,” alisema Gwajima na kuongeza:
“Sasa Mbasha alipotoka huko alikokimbilia na kusikia kuwa mkewe yuko hapa kanisani, ndipo alipoanza kueneza uzushi,” alisema.

Gwajima alisisitiza kuwa Flora hakufikia kwake kwa jambo lolote bali aliendelea kuishi katika nyumba aliyopanga.
Alipoulizwa kwa nini hamshitaki Mbasha ili kulinda heshima yake, Gwajima alisema ameshawaita ndugu zake akiwemo baba yake mzazi lakini nao wakaonekana kutommudu Emmanuel.
“Nilishawaita wazazi wake, baba na mama yake, ndugu zake kina Mbasha na tukazungumza. Lakini baba yake alisema hata yeye amemshindwa. Yaani anawadharau hata ndugu zake,” alisema.
Akisimulia jinsi alivyokutana na Emmanuel na Flora Mbasha, Mchungaji Gwajima alisema awali walikuwa wakiimba kwenye mikutano aliyokuwa akihubiri.
“Hawa hawakuwa washirika wetu, ila walikuwa wakija kuimba kwenye mikutano yetu ya Injili. Walikuja Arusha, Moshi na Tanga, kwa hiyo tulikuwa tukiwatumia sana. Baadaye ndiyo yakatokea hayo hadi Flora akakimbilia kanisani kwetu,” alisema.

Hata hivyo Gwajima alisema hakujua kama Flora ni mjamzito wakati anakuja kuomba msaada kanisani kwake.

“Mimi sikujua kama alikuwa mjamzito, hata taarifa kwamba amejifungua ndiyo nazisikia kwako. Hapa nimetoka ‘airport’, sikuwepo Dar es Salaam,” alisema na kuongeza:
“Sasa kama mtu una wasiwasi na mtoto si ukapime DNA ili upate uhakika? Hii ni habari ya kutaka tu kulichafua kanisa na huduma,” alisisitiza.

Flora anena
Gazeti hili lilimtafuta Flora kwa njia ya simu ili kuzungumzia suala hilo ambapo alisema “Siko tayari kuzungumza lolote kuhusu Mbasha kwa sasa. Yeye anajeuri ya pesa ndo maana anafanya haya yote lakini mimi ninasimama na Mungu wangu na ninajua Mungu atanipigania,” alisema Flora.
Alipoulizwa kuhusu hali ya mtoto wake mchanga, alisema “Mtoto hajambo, lakini mtoto anayesambazwa kwenye mitandao siyo wangu, na hizo picha nyingine nafikiri ni za kutengeneza tu,” alisema Flora.

Mbasha
Kutokana na hali hiyo MTANZANIA ilimtafuta mume wa Flora, Emmanuel Mbasha, ili kuzungumzia suala hilo, licha ya kupokea simu yake ya kiganjani, aliishia kusema yuko njiani hivyo apigiwe baadaye.

Hata alipopigiwa baadaye, aliendelea kusema kuwa atafutwe baadaye na wala hakujibu ujumbe wa simu (sms).

Alipotafutwa kwa njia ya ujumbe mfupi wa WhatsApp, ujumbe huo ulionekana kufika na kusomwa na baada ya muda alituma ujumbe wa sauti uliokuwa na wimbo na kuandika maneno mafupi yaliyosomeka ‘wimbo wangu mpya’.

Pamoja na mambo mengine, wimbo huo unamaneno yasemajo “Haribu mipango ya shetani, haribu…, Binadamu wengine mashetani mfano wa Cobra, wanawaza mabaya, kuna siku watakufa kabisa,” ulisikika ujumbe wa wimbo huo