Msanii anayetesa katika mziki wa kizazi kipya hapa nchini,
Nassib Abdul 'Diamond Platnumz' usiku wa jumamosi iliyopita
alijikuta katika wakati mgumu baada ya kuzomewa na mashabiki
kwenye viwanja vya Leaders Jijini Dar es Salaam.
Mbali ya kuzomewa, Diamond pia alirushiwa chupa za maji ambazo
zilileta kadhia, lakini Diamond alionekana akiwahimiza madancer
wake wafanye kazi iliyowapeleka pale licha ya zomeazomea kuzidi
uwanjani.....
Msanii huyo alipoona vitendo vya kutaka kumkwamisha asiimbe
vikiendelea, aliamua kuwamwagia fedha mashabiki hao, ndipo wakaacha
kuzomea na kuanza kugombea fedha hizo kisha kuanza
kumshangilia....
Baadhi ya wadau walisikika wakidai, kundi hilo lililokuwa
likimzomea liko upande wa mmoja wa wasanii mahiri hapa
nchini.Wasanii wengine walioonja joto ya jiwe ni pamoja na
Khamis Mwinjuma 'Mwana FA' na Ambwene Yesaya 'AY'.
Aidha, baadhi ya mashabiki walilaani vikali tukio hilo la
kumzomea Diamond na kumrushia chupa za maji ambazo inadaiwa
zilikuwa na haja ndogo ndani yake.
Mashabiki hao walisema tukio hilo halipendezi na linapaswa
kukemewa na kuwataka waratibu pamoja na jeshi la polisi
kuzidisha ulinzi katika matamasha makubwa kama hayo.
Hii ni mara ya pili kwa Diamond kuzomewa,tukio la kwanza
likiwa kilele cha tamasha la Fiesta mwaka jana kwenye viwanja
hivyo.